Paul Pogba tayari kwa mazoezi


Kiungo nyota na mchezaji mahiri wa Man United Paul Pogba ameonyesha dalili za kupona haraka kuliko ilivyotarajiwa majeraha yaliyokuwa yakimsumbua
Manchester United wameanza kupata raha kwani kiungo wao nyota Paul Pogba ameanza kurejea mazoezini, akianza kwa mazoezi mepesi, mwezi mmoja tu baada ya kupata majeraha.
Mchezaji huyo wa kimataifa wa Ufaransa alipata majeraha ya misuli ya paja United ikishinda 3-0 dhidi ya Basel Septemba 12, hivyo kusababisha hofu ya kumkosa hadi mwisho wa mwaka.
Bosi wake, Jose Mourinho amethibitisha kuwa United itakuwa bila ya Pogba, 24, kwa "muda mrefu", akikataa kusema dhahiri ni lini mchezaji huyo atarejea kwenye kikosi chake.
Pogba amepona kwa haraka kuliko ilivyotarajiwa, hata hivyo, imebainika baada ya kufanya mazoezi mepesi kwenye gym akiwa kwenye mapumziko mafupi Florida.
Mchezaji huyo wa zamani wa Juventus alitupia chapisho la Instagram kuwajulisha wafuasi wake jinsi anavyoendelea, akitupia idadi ya video zikionyesha akiwa anakimbia kwa mashine na kutembea ndani ya gym.
Ripoti zinadai kuwa Ufaransa wanatarajia kuwa na Pogba kwenye kikosi chao kabla ya mapumziko mengine ya kimataifa, yatakayokuwa mapema mwezi Novemba.

No comments: