Makamu wa rais wazozana kuhusu madai ya sumu Zimbabwe



Makamu wa rais wa Zimbabwe Phelekezela Mphoko amemlaumu hadharani makamu mwenzake wa rais Emmerson Mnangagwa, akimshutumu kwa kujaribu kuliyumbisha taifa hilo.
Matamshi hayo yanajiri baada ya bwana Mnangagwa kudai kuwa aliwekewa sumu.
Chama tawala cha Zanu-PF kimekuwa kikijaribu kukabiliana na hali ya wasiwasi ndani ya chama hicho miongoni mwa makundi pinzani yanayotaka kumrithi rais Mugabe mwenye umri wa miaka 93.
Bwana Mnangagwa na mke wa rais Grace Mugabe wanaonekana kuwa watu walio kifua mbele katika siasa za kumrithi rais huyo .
Katika taarifa kwa vyombo vya habari , bwana Mphoko alimshutumu mwenzake kwa kudanganya kuhusu kuwekewa sumu mnamo mwezi Agosti.
Bwana Mphoki kwa sasa ndiye kaimu rais kwa kuwa rais Mugabe hayupo nchini humo.
Bwana Mnangagwa alikuwa mgonjwa mnamo mwezi Agosti katika mkutano wa hadhara ulioongozwa na rais Mugabe na akalazimika kusafirishwa kwa ndege hadi nchini Afrika Kusini.
Wikendi iliopita , bwana Mnangagwa alisema kuwa mtu alijaribu kumwekea sumu katika chakula chake.
Wafuasi wake wanasema kuwa kundi pinzani katika chama tawala cha Zanu PF ndio la kulaumiwa na kudai kulalamikia Ice crème kutoka kwa shamba la rais Mugabe.
Amesema kuwa madai hayo ya hivi karibuni yanaonyesha ajenda ya kutaka kuhujumu mamalaka ya rais na kuzua wasiwasi katika chama.

No comments: