Mabingwa wapya STARTIMES RBA ni Savio kwa wanaume na Vijana Queens kwa wanawake



TIMU  ya Mpira wa Kikapu ya Savio  imekuwa mabingwa wa Ligi ya Kikapu Mkoa wa Dar es Salaam kwa upande wa wanaume (Dar e Salaam Stertimes RBA) kwa mwaka 2017 baada ya kuwachapa mabingwa watetezi JKT Mgulani kwa pointi 88 dhidi ya 81 katika fainali iliyopigwa jana kwenye uwanja wa ndani wa Taifa.
VIJANA QUEENS WANAWAKE NA SAVIO WANAUME MABINGWA WAPYA STARTIMES RBA MSIMU WA 2017-18Fainali hiyo ilikuwa ni ya shindano la 33 ambapo bingwa huyo mpya alikabidhiwa zawadi ya sh. 700,000 na Medali za Dhahabu huku JKT ambaye ni mshindi wa pili akipatiwa sh. 500,000  na medali.

Aidha kwa upande wa kina dada bingwa amekuwa ni Timu ya Vijana Queens. Imetwaa ubingwa huo baada ya kuichapa Timu ya Donbosco kwa pointi 72 dhidi ya 69.

Kwa huo Vijana Queens pia wamekabidhiwa kitita cha sh.700,000 na medali za Dhahabu huku Donbosco wakikabidhiwa sh. 500,000 na medali.

Washindi wa tatu kwa pande zote wamepatiwa sh.300,000 kila mmoja ambapo kwa wanaume ni Vijana City Bulls huku kwa wanawake ikiwa ni JKT Stars.

Akizungumza katika hafla ya kukabidhi zawadi kwa washindi Makamu wa Rais wa Kampuni ya StarTimes nchini Zuhura Hanif,  amesema kupitia udhamini wa RBA ni mwanzo wa kuwa karibu na jamii kwa kuwapa vijana ajira kupitia michezo.
“Huu ni mwanzo wa kuwa karibu na jamii, lakini pia kuwapa vijana ajira pamoja na kuwapa nafasi ya kuonyesha vipaji vyao,” amesema Hanif.

Aidha ametoa wito kwa kampuni nyingine ambazo zipo tayari kusaidia maendeleo ya mpira wa kikapu nchini kujitokeza ili kusaidia vijana kupata ajira pamoja na kuonyesha vipaji vyao.

Kwa upande wa ligi ya kikapu daraja la kwanza Timu ya Kigamboni ndiyo mabingwa na kutokana na ubingwa huo wamepanda katika Ligi ya Mkoa ya RBA katika msimu ujao.

No comments: