Aokota bomu na kulificha akidhani lina dhahabu ndani

Wananchi waishio pembezoni mwa milima ya vijiji vya Mwamapalala na Nshantiba mkoani Shinyanga wamedaiwa kuokota mabomu na kuyahifadhi wakidhani kuwa ni dhahabu.
Milima hiyo ambayo ipo katika hifadhi ya Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), na ni maalumu kwa ajili ya kufanyia mazoezi, wananchi wamedaiwa kuokota mabomu yaliyogoma kupasuka na kuyaficha ndani wakiamini yana dhahabu.
Mkuu wa kikosi cha Jeshi cha 82, Luteni Kanali George Kyamba, ametoa taarifa hiyo kwenye mkutano wa hadhara wa Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Josephine Matiro, uliokua na lengo la kutoa elimu kwa wananchi kuacha tabia ya kuvamia maeneo ya jeshi.
Wiki iliyopita mwananchi mmoja katika vijiji hivyo aliokota bomu na kwenda nalo nyumbani kwake ambapo, Kyamba amesema wa walipokuwa wakilitafuta bomu hilo, walipewa taarifa na msamaria mwema kuwa kuna mwananchi alilichukua na kwenda kulificha nyumbani kwake, akidai kuwa akilipasua atakuta dhahabu.
Hata hivyo, Kyamba amesema walipomfuata aligoma kulitoa bomu hilo hadi walipotumia nguvu ya ziada.
Tayari mtaalamu wa mabomu na milipuko wa Jeshi hilo, Meja Siraji Balekao, amesema wameshaliharibu.

No comments: