Serikali yapewa saa 72 kuwashtaki maafisa wa IEBC Kenya

Mwenyekiti wa tume ya IEBC Wafula Chebukati
Upinzani nchini Kenya Nasa umempatia mkurugenzi wa mashtaka nchini humo Keriako Tobiko saa 72 kuwafungulia mashtaka maafisa wa IEBC wanaotuhumiwa kuharibu uchaguzi wa Agosti 8.
Wakati huohuo upinzani huo umeapa kuwafungulia mashtaka ya kibinafsi maafisa hao wa IEBC.
Nasa imesema kuwa mahakama ya juu siku ya Jumatano haikuwaondolea lawama maafisa wa IEBC na kwamba ni sharti washtakiwe kwa kufanya udanganyifu katika uchaguzi huo.
''Kufuatia uamuzi uliotolewa na mahakama ya juu, afisi yako imesema kwamba inaangazia uamuzi huo kwa kina na kufanya uamuzi wa iwapo itawafungulia mashtaka ya uhalifu maafisa wa IEBC au la.Uelewa wetu ni kwamba makamishna na wafanyikazi wakuu wa IEBC walitekeleza uhalifu'', alisema Mbunge Mathare MP Anthony Olouch.
Kiongozi wa upinzani amempatia mkurugenzi wa mashtaka saa 72 kuwafungulia mashtaka maafisa wa tume ya uchaguzi wa IEBC
Aliongezea: Kutokana na uchaguzi wa marudio uliotangzwa kufanyika tarehe 26, kctoba 2017, maafisa waliorodheshwa hapa chini hawataruhusiwa kusalia afisini ili kuendeleza uhalifu waliotekeleza.Na hadi pale uchunguzi kuhusu uhalifu uliotekelezwa na maafisa hao utakapofanywa na mashtaka kufunguliwa dhidi yao baada ya saa 72, sisi tutawashtaki kulingana na kifungu cha 28 ya mshataka ya umma.
Maafisa wa IEBC ambao Nasa inataka wafunguliwe mashtaka ni pamoja na afisa mtendaji Ezra Chiloba, mwenyekiti Wafula Chebukati, Betty Nyabuto, Immaculate Kassait, James Muhati, Praxedes Tororey ambaye amejiuzulu, Moses Kipkogei, Abdi Guliye, Molu Boya na Marjan Marjan.

No comments: